Pages

Sample Text

Frank Kimaro run this blog

11/19/2011

JK apingana na hoja za Chadema amtupia kombora Mbowe

ASEMA ATATIA SAINI BILA SHAKA YOYOTE

RAIS Jakaya Kikwete emesema licha ya kelele za wanasiasa, atasaini Sheria ya mchakato wa kuunda Katiba Mpya.
Alitoa kauli jana na kupangua hoja zote kupinga mchakato huo zilizotolewa na Chadema kwamba muswada huo haukuzingatia kanuni zitakazowezesha demokrasia.Kauli hiyo ya Rais imekuja saa chache baada ya Bunge kupitisha Muswada wa Mabadiliko ya Katiba ambao ulisusiwa na Wabunge wa Chadema na NCCR-Mageuzi kwa madai kuwa mchakato mzima una kasoro.

Akizungumza na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam katika Ukumbi wa PTA, Sabasaba juu ya hali ya uchumi nchini na mchakato wa Katiba, Rais Kikwete alisema atatia saini sheria ya mchakato wa kuunda katiba mpya ambayo inatokana na muswada uliopitishwa na Bunge jana.

Alikibebesha lawama nyingi Chadema kwa kile alichosema ni upotoshaji wa mchakato huo kwa lengo la kuuvuruga wakati unaendeshwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.

Alimtupia shutuma za waziwazi Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akisema amekuwa kigeugeu kwa sababu mwanzo alimsifu (Rais Kikwete), kwa kukubali Katiba kubadilishwa lakini baadaye akageuka na kuanza kumponda.

“Mbowe ni miongoni mwa watu walionimwagia sifa baada ya kutangaza nia yangu ya kuanza kwa mchakato wa Katiba Mpya, nakumbuka ilikuwa Februari 11, mwaka huu wakati akichangia hotuba yangu katika Kikao cha Bunge alisema: ‘Tunampongeza Rais katika suala hili.’ Ila muda mfupi baadaye chama chake kikaja na mtizamo tofauti wa kunyang’anywa hoja yao… na kwamba Rais asiunde tume wala kuhusika katika mchakato.”

Alisema alishangazwa na kauli za Chadema na kusema: “Hii si mara ya kwanza kwa nchi yetu kufanya zoezi la marekebisho ya Katiba na hata kuandika Katiba Mpya.”

Alisema kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi, katika suala la upatikanaji wa Katiba anayeunda tume ni Rais na akisema hata katika utawala wa Awamu ya Kwanza na ya Pili, ilibadilishwa mara tatu na Rais ndiye aliyeunda tume.

“Mwaka 1977 yalifanyika mabadiliko mengine ya Katiba ambayo yalitengeneza Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ilikuja kufanyiwa marekebisho makubwa mwaka 1984,” alisema Rais Kikwete.

Mwaka 1991 na 1992, alisema iliundwa tume nyingine iliyoongozwa na Jaji Francis Nyalali ya kukusanya maoni ya Katiba ya kutoka mfumo wa chama kimoja kwenda vyama vingi.

“Tume hii ilipendekeza sheria 40 zifutwe, zilifutwa na nyingine zinaendelea kufutwa ikiwemo sheria ya kumweka mtu kizuizini,” alisema.

Alisema mwaka 1997 katika utawala wa Rais Benjamin Mkapa aliundwa Tume ya Jaji Kisanga ambayo ilikusanya maoni ya mabadiliko ya 13 na 14 ya Katiba.
“Siku zote katika mchakato wa Katiba, tume huundwa na Rais, sasa iweje sasa?... Rais amepungukiwa sifa kikatiba?” alisema na kusisitiza kwamba ndiye mwenye mamlaka kikatiba kuunda kamati hiyo.
Alisema iwapo Chadema kitaandaa mchakato wake wa kuunda katiba itabidi mawazo yao wayakabidhi kwa kamati atakayoiunda.
Alisema tayari CUF iliwasilisha rasimu yake ya Katiba na kuikabidhi serikalini na kwamba nayo itapelekwa kwenye kamati kama sehemu ya maoni yaliyotolewa na makundi ya Watanzania.
Rais alisema uteuzi wa wajumbe katika tume utazingatia sifa na kwa mujibu wa kanuni akisema hana mamlaka ya kuichagua kwa kuzingatia vigezo vya urafiki.
Isitoshe, alisema kitendo chake cha kuridhia mabadiliko ya Katiba nchini kwa sasa hakina maana kwamba iliyopo haifai. Alisema iliyopo imeiongoza vizuri nchi na kuwa kwenye utulivu na amani kwa miaka 50, hivyo haipaswi kuonekana kuwa haifai: “Lengo la kutaka mabadiliko hayo ya Katiba ni kuunda mpya itakayoendana na matakwa ya Watanzania katika wakati huu ambao wanatimiza miaka 50 tangu uhuru wao.”
Alisema Katiba itakayoundwa itajumuisha mawazo ya Watanzania wote ili kuhakikisha kuwa italiongoza vyema taifa katika miaka mingine 50 likiwa tulivu na lenye mshikamano.
Rais kuwa dikteta
Alisema kauli kuwa anaongoza kwa kutumia mtindo wa kidikteta ni za kizushi akisema endapo ingekuwa hivyo, angewatia kizuizini watu wengi ambao wanatoa hoja za kupotosha mambo yanayotendwa na Serikali yake.
Badala yake alisema amekuwa mvumilivu wa yote kwa kuwa anajua wazi katika nchi inayoongozwa kidemokrasia, lazima kuwepo na tofauti za mawazo. Alisema angekuwa hivyo, hata wanaomwita dikteta wasingethubutu kutamka hayo maana wangekamatwa na kutiwa kizuizini au kupotea katika mazingira utata.
Alikigeuzia kibao Chadema akisema kama ni udikteta basi ndicho chenye sifa hiyo kwa kuwa viongozi wake wamekuwa hawataki kuzingatia demokrasia kwa kulazimisha mambo.
Alisema kuwa amekuwa akishangazwa na kauli za Chadema akitoa mfano wa iliyotolewa na chama hicho kuwa kama Katiba mpya haitaandikwa kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao 2015... “Patakuwa hapatoshi.”
Akasema lakini hata pale alipokubali mchakato wa kuunda katiba hiyo kabla ya mwaka 2015, ili ‘patoshe’ bado Chadema kimekuja na kauli nyingine mchakato huo ukiendelea kuwa “Patakuwa hapatoshi.”
Muswada wapita
Awali, jana mchana wakati kazi ya kupiga kura ikianza ili kupitisha muswada huo, wabunge wa Chadema na NCCR Mageuzi, hawakuwepo ndani ya Ukumbi wa Bunge kwa kwani walitoka muda mfupi baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na majibu wakiendeleza msimamo wao wa kupinga muswada huo.
Baada ya kuwahoji wabunge, Spika wa Bunge, Anne Makinda alisema: “Muswada umepita na sasa tunasubiri Rais aweke mkono wake ingawa wapo wanaosema aukatae sasa sijui wana maana gani...” alisema na kushangiliwa na wabunge.

Kabla ya kupitishwa, muswada huo ulifanyiwa marekebisho kadhaa yaliyotokana na hoja zilizotolewa na wabunge ambao waliitaka Serikali kuvifanyia marekebisho baadhi ya vifungu vyake.

Makinda aliwaponda wabunge waliosusia mjadala wa kupitishwa kwa muswada huo akisema kitendo hicho si cha kiungwana.

Alisema kulingana na nafasi zao, alitegemea kwamba wangehudhuria vikao hivyo na kutoa hoja mbadala ili wananchi wajue kile wanachokilalamikia.

“Nilitegemea kuwaona katika vikao ili watoe maoni yao kuhusu muswada huu na wapi palipokosewa kuliko kutoka nje. Sasa wananchi watajua sababu ya wao kususia jambo hili?”

Viongozi wa dini waonya

Wakati Bunge likipitisha Muswada wa Marekebisho ya Katiba jana, baadhi ya viongozi wa dini wameponda hatua hiyo wakisema Serikali haikuwatendea haki Watanzania kwa kuwa hatua hiyo imelazimishwa.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili jana viongozi hao walisema Serikali ilipaswa kusikiliza hoja za wapinzani na wanaharakati waliotaka muswada huo usomwe bungeni kwa mara ya kwanza na siyo mara ya pili.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Methodius Kilaini alisema Serikali ilipaswa kufuatilia suala hilo kwa wananchi kabla ya kuupitisha muswada huo vinginevyo ilichofanya jana, ni kupitisha matakwa yake.

“Serikali haikutakiwa kuupitisha muswada huo kwa sababu wananchi hawajatoa maoni ya kutosha. Muswada huo ulipaswa kurejeshwa kwa wananchi ili watoe maoni yao ili katiba itakayotengezwa iwe inayojitosheleza,” alisema Askofu Kilaini.

Askofu Kilaini alisema Muswada wa Katiba Mpya, hauwezi kupitishwa kwa matakwa ya watu wachache akisema ni lazima wananchi washirikishwe.

Kauli ya Kilaini iliungwa mkono na Katibu wa Umoja wa Makanisa ya Kipentekoste Tanzania, Mchungaji Leonard Mtaita aliyesema kuwa mchakato huo ni jambo jema lakini, akaonya kwamba mgawanyiko uliojitokeza katika hatua za awali ni hatari.

“Kuwa na tofauti za kimtazamo katika jambo hili ni suala la kawaida, lakini mgawanyiko katika hatua hizi za awali ni hatari kwa taifa na unaweza kusababisha hata lengo lililokusudiwa kutofikiwa,” alisema Mtaita.

Alisema ni wajibu kwa Serikali kuhakikisha Watanzania wanadumisha umoja katika mchakato huu wa kuandika upya Katiba ya nchi ili malengo yaliyokusudiwa yafikiwe.

Mtaita alimtaka Rais Jakaya Kikwete kutumia hekima zake katika kufanikisha jambo hilo kwa sababu muswada huo haupingwi tu na watu waliosusa kuhudhuria vikao bungeni, bali pia na makundi mengine ya watu wakiwamo wataalamu.

Alishauri Rais kuunganisha makundi hayo kwa kuwaleta karibu viongozi wastaafu na wanaharakati ili kupata muafaka wa Katiba Mpya.

Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum alitaka Serikali kuzishirikisha kikamilifu taasisi za dini nchini katika mchakato huo ili watoe mchango wao katika kuwaelimisha waumini... “Kama taasisi za dini zitapewa nafasi kushiriki katika suala hili la Katiba, tunaweza kuisaidia Serikali kupata mawazo mazuri ambayo yatachangia kuleta Katiba itakayojitosheleza na itakayojenga umoja na kuleta maendeleo ya taifa.”

Sheikh Salum alisema baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakitumia fursa ya kuundwa Katiba Mpya kujitafutia umaarufu kisiasa akisema jambo hilo si jema kwa mustakabali wa taifa.

“Suala la uundwaji wa Katiba mpya ni muhimu. Linatakiwa kuangaliwa kwa umakini, sasa watu wanapoanza kutumia uundwaji wa katiba hiyo kujijenga kisiasa inaweza kuleta athari kubwa kwa taifa,” alisema.

Aliwataka wananchi kuheshimu Bunge kwa sababu ndicho chombo kinachotunga sheria za nchi badala ya kufanya uamuzi wa kishabiki na kusababisha kutoweka kwa amani ya nchi.

11/18/2011

Wanaharakati wasema endapo katiba itasomwa maandamano yatafanyika nchi nzima.


  • Wanaharakati wageuka mbogo,watoa onyo kali
  • Watishia kuitisha maandamano yasiyo na kikomo
  • Ni endapo Muswada wa Katiba utasomwa leo
  • Wasema hakuna polisi, mgambo atakayewauzia
Akizungumza wakati wa kuhitimisha mjadala wa Katiba uliofanyika jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania, Deus Kibamba, alisema njia pekee ya kuepusha maandamano hayo ni Serikali kusoma Muswada huo kwa mara ya kwanza na si mara ya pili kama ambavyo imekwishatangaza.
“Napenda kuwaambia ndugu washiriki kama kesho (leo), Serikali itasoma Muswada huu kwa mara ya pili, tutaitisha maandamano ya nchi nzima yasiyokuwa na kikomo.
“Tarehe na siku tutawaambia muda si mrefu, tunataka kuona muswada huu unasomwa kwa mara ya kwanza ili Watanzania wapate fursa ya kuujadili,”alisema Kibamba na kupigiwa makofi.
Alisema Jukwaa la Katiba litaongoza maandamano hayo, ambayo lengo lake ni kupinga jeuri ya Serikali.
“Inasikitisha kuona viongozi wa Tanzania ni waoga mno, nawahakikishia kwamba  maandamano ya katiba yatatisha, hatuogopi  polisi, mgambo wala  wanasiasa watakaozuia dhamira yetu,”alisema Kibamba.
Wakichangia kongamano hilo kwa nyakati tofauti, wanaharakati na washiriki wa mjadala huo, walisema viongozi  hawajifunzi wala kuonyesha uzalendo, zaidi ya kujadili posho na marupurupu, huku wakishindwa kuwatetea wananchi.
“Wabunge waache kushabikia Serikali ya kikoloni, tunataka waitetee Tanzania, sisi ndio tunaowapa mamlaka ya kwenda mjengoni (bungeni), kama kesho (leo) watausoma Muswada huu kwa mara ya pili, tutadai haki yetu barabarani bila kuogopa chochote,
“Tutakapofanya maandamano hatutahitaji polisi, zile bunduki na mabomu ya machozi na maji ya kuwasha, wakawapigie mafisadi ambao wanatumia fedha za walipa kodi kwa maslahi yao,”alisema Paulina Makuli.
Naye  Renatus Pamba, alisema wingi wa wabunge wa Chama Cha Mapinduzi(CCM), unatia wasiwasi kwani huenda kukawa na kura nyingi za kutaka kupitisha Muswada huo usomwe mara ya pili kwa maslahi binafsi.
Alisema kamwe hawataogopa kudai haki yao, kwani miaka 50 ya kuburuzwa na hali ngumu ya maisha  imefikia kikomo.
“Tunawashangaa sana hawa viongozi wetu, mbona wanapokuja kuomba kura hawatwambii sisi walemavu tusiwapigie, ndiyo kwanza wanakusogeza karibu na kukuonyesha majina ya viongozi na vyama vyao, kwa nini wakati wa kuandika Muswada huu hawakutuwekea mazingira rafiki katika usomaji, au sisi siyo Watanzania, ”alihoji mmoja wa wanaharakati hao, Maria Charles.
…Tunawaomba viongozi wetu watutambue makundi maalum katika uandishi wa muswada  huo kwa kutumia nukta nundu ili na sisi pia  tuweze kusoma bila kuhitaji msaada wa mtu yeyote,”alisema
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba mpya, unatarajiwa kusomwa kwa mara ya pili na tatu bungeni leo huku wananchi na wanaharakati wakizidi kuupinga.

CHADEMA wamuambia spika asiingilie mambo ya ndani ya chama hicho.

 
Katika kauli hiyo, Makinda anadaiwa kunukuliwa na vyombo vya habari akisema wabunge wa Chadema hawakuwatendea haki wananchi waliowatuma bungeni kutokana na uamuzi wao wa kususia mjadala huo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu wa Wabunge wa chama hicho, John Mnyika, alisema Spika Makinda siyo msemaji wa wapiga kura wao na amemtaka ashughulike na wapiga kura wa jimbo lake la Njombe Kusini.
Mkutano huo, ulihudhuriwa pia na Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu.
“Tumetafakari hoja zinazoendelea kujengwa kwamba wabunge wa CHADEMA hawakuwatendea haki wananchi waliowatuma kuwawakilisha bungeni kutokana na uamuzi wetu wa kususia mjadala wa Katiba.
“Tunamtaka Spika ajue yeye si msemaji wa wapiga kura wetu, waliotuchagua wanatuamini na wanatupigia simu kwamba wanakubaliana na uamuzi wetu.
“Kama tungekubali muswada usomwe kwa mara ya pili, ingekuwa hatujawatendea haki wapiga kura wetu, lakini uamuzi wetu huu ndiyo msimamo wa wananchi katika suala hili, Spika ashughulike na wapiga kura wa jimbo lake,” alisema Mnyika.

Mbali na hilo, Mnyika pia alimgeukia Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashilila na kupinga kauli iliyotolewa na kiongozi huyo wa Bunge jana kupitia vyombo vya habari.
Katika maneno hayo, Dk. Kashilila anadaiwa kupinga uamuzi wa wabunge hao na kusema walipaswa kutumia kanuni ya 86 ya Bunge inayoruhusu mbunge kutoa hoja ya kuliomba Bunge au mjadala wa siku husika uahirishwe badala ya kususia.
“Tulimsikia Kashilila akisema tumeshindwa kutumia kanuni ya 86 (3) inayoruhusu mbunge kutoa hoja ya kutaka mjadala uahirishwe.
“Kauli hii inatoa picha kuwa, Kashila ametumwa na CCM au Serikali kufanya propaganda, Kashilila anatakiwa kufanya kazi yake ya kitaalamu au ya kiutendaji kama kiongozi wa mhimili wa Bunge.

“Kashilila ni mwongo, mimi nilisimama mara tatu nikitumia kanuni hiyo hiyo ya 86 kuomba mjadala uahirishwe, lakini Spika alininyima fursa wala hakutaka kuwauliza wabunge, akaangalie taarifa rasmi za kumbu kumbu za Bunge,” alisema Mnyika.
Katika hatua nyingine, Mnyika alisema Kamati Kuu (CC) ya chama chake itakutana Novemba 20, mwaka huu kujadili Muswada wa Katiba mpya ili kupanga utaratibu wa kwenda kwa wananchi.
Hata hivyo, Mnyika alisema wabunge wote wa Chadema watashiriki mkutano huo bila kujali ni wajumbe au laa na kwamba kutokana na kikao hicho baada ya Bunge kuhitimishwa Ijumaa wiki hii, wabunge wote wa chama hicho hawatashiriki shughuli nyingine za Bunge ikiwamo semina ya Jumamosi.
“Kwa maneno hayo ndiyo kusema kwamba, Jumamosi asubuhi wabunge wote wa CHADEMA tutaelekea Dar es Salaam kwa ajili ya kikao hicho kitakachofanyika siku ya Jumapili,” alisema.
Wakati huo huo, mjadala wa Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba jana uliendelea, ambapo baadhi ya wabunge walituhumu baadhi ya mabalozi na wafadhili kwamba wanashirikiana na wanaharakati na wanasiasa kutaka kuvuruga nchi.
Mbunge wa Sumve, Richard Ndassa (CCM), ndiye aliyewashambulia mabalozi hao, akisema kuwa, wapo baadhi ya mabalozi hapa nchini ambao hawana nia njema na Watanzania.

“Hawa mabalozi wanatakiwa kutambua kwamba, wanatakiwa kuwaachia Watanzania waamue mambo yao yakiwamo haya ya kupata Katiba mpya pindi mchakato utakapoanza.
“Kwa bahati mbaya, kuna baadhi ya mabalozi wanaonekana kushirikiana na baadhi ya wanasiasa na wanaharakati kwa nia ya kuhakikisha amani iliyopo inatoweka jambo ambalo Serikali inatakiwa kuwa makini,” alisema Ndassa.

SAID MTANDA
Mbunge wa Mchinga, Said Mtanda (CCM), pamoja na mambo mengine, alitumia fursa hiyo kutoa angalizo kwa Serikali kuwa makini na baadhi ya wanaharakati ambao wanaonekana kukosa dhamira nzuri.
Mtanda alionyesha wasiwasi kwa wanaharakati hao huku akisema wapo baadhi ya wafadhili kwa masharti yanayolenga kuwagawa Watanzania.
“Hao wanaharakati ndiyo ambao wamekuwa wakitoa mawazo hasi kwa Watanzania, baadhi ya wafadhili hawa wanatumia nafasi yao kufadhili baadhi ya wanaharakati kwa ajili ya kufanikisha mitazamo na malengo,” alisema Mtanda.
ANDREW CHENGE
Mbunge wa Bariadi Magharibi, Endrew Chenge (CCM), alisema kazi inayofanywa na wabunge kwa sasa ni sawa na kujenga barabara na kwamba kazi hiyo itafanikisha mchakato wa kupatikana Katiba mpya.
Chenge, aliwapiga vijembe wabunge wa CHADEMA, akisema ni jambo la kusikitisha kuwa baadhi ya kikundi cha watu wakijifanya wao ndiyo wana mawazo yanayofaa kuliko wengine.
Mjadala wa muswada ambao kwa mujibu wa ratiba ya Bunge ulikuwa uhitimishwe jana, umesogezwa mbele ambapo unatarjiwa kuendelea tena leo. Kwa mujibu wa Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani, hatua hiyo ni kutokana na ongezeko la wabunge kutaka kuuchangia.
BAVICHA YAKUNJUA MAKUCHA

Katika hatua nyingine, Baraza la Taifa la Vijana la CHADEMA (BAVICHA), limetangaza kupambana  na wabunge wa CCM, wanaounga mkono Muswada wa Katiba mpya kusomwa bungeni kwa mara ya pili.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa BAVICHA, John Heche, alisema chama chake kiko tayari kupambana hadi kufa kwa ajili ya kuwatetea Watanzania na sasa wanaanza kazi ya kuzunguka katika majimbo ya wabunge wa CCM walionekana kutetea muswada huo ingawa umepingwa na vikali na wanaharakati.
“Muswada uliosomwa juzi kwa mara ya pili ni batili, kwa kuwa ulipaswa usomwe kwa mara ya kwanza, sasa tutaangalia wabunge wote ambao wameonekana kuuunga mkono, hao ndiyo tunaanza nao kwa kuzunguka kwenye majimbo yao kuhamasisha vijana na wafuasi wetu  wakatae sera zao na udhalimu unaofanywa na Serikali ya CCM.
“Muswada uliosomwa kwa mara ya pili bungeni ni mbovu kuliko hata ule wa kwanza kwani baadhi ya mambo yameongezwa, mambo kandamizi yote yaliyokuwa kwa mara ya kwanza hayakuondolewa.
“Kitendo cha kulazimishwa kusomwa kwa mara ya pili, ni ujanja ujanja wa Serikali ya CCM na maswahiba wao, wenye nia ya kutaka kuzalisha Katiba itakayolinda maslahi yao na siyo matakwa ya wananchi.
“Katika hili BAVICHA itatoa kazi wa Jeshi la Polisi kwani  hivi sasa  jeshi hilo limeonekana kutokuwa na kazi ya kufanya zaidi ya kupambana na wafuasi wetu pamoja na wafanyabiashara ndogo ndogo (Wamachinga).
“Jeshi la Polisi linaonekana halina kazi ya kufanya, wameshindwa kuwakamata watumuhiwa mbalimbali  nchini, kazi yao kubwa imebaki kupambana na CHADEMA, tunasema tutawapa kazi ya kufanya kwani tutafanya maandamano makubwa kwa wakati mmoja  tuone watajigawa vipi.
“Katika  vurugu za Mbeya kuna askari polisi walitolewa  maeneo mengine kwa ajili ya kuongeza nguvu, sasa haya maandamano yanayokuja sijui watajigawa vipi,” alisema Heche.
AWAONYA UVCCM
Katika hatua nyingine, Heche amemtaka Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana CCM (UVCCM), Martin Shigela, kuacha kulinganisha vijana wa Chadema  na UVCCM.
“Juzi juzi nilimsikia Shigela akihamasisha vijana wa UVCCM, kujitokeza kutulaani, tunapenda kuwaambia hatubabaiki kabisa, namuomba Shigela apange maandamano tukutane aone namna patakavyochimbika,” alisema Heche.
Kuhusu  halmashauri zinaozoongozwa na Chadema, alizitaka zitenge maeneo ya wafanyabiashara ndogondogo ili wafanye biashara zao bila usumbufu.

11/16/2011

Zitto asema bila muafaka njia mbadala itafuatwa.



WAKATI mjadala wa Muswada wa Sheria ya Kuunda Katiba Mpya ukizidi kuitikisa Serikali, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe ameonya kwamba kama suala hilo litachezewa, chama chake kitatafuta njia mbadala kwa wananchi ya kupata Katiba. Mjadala kuhusu muswada huo unakabiliwa na upinzani mkali kutoka ndani na nje ya Bunge na jana wabunge wengi wa CCM waliochangia, waliwashambulia wenzao wa Chadema.

Wabunge hao wa CCM, juzi walifanya kikao cha chama hadi saa 6:00, pamoja na mambo mengine kujadili namna ya kupitisha muswada huo. Kamati Kuu ya Chadema nayo ikikutana kwa dharura kujadili suala hilo. Zitto ambaye amerejea siku tatu zilizopita akitokea India alikokuwa akipatiwa matibabu, alisema jana katika mahojiano maalumu na gazeti hili kwamba, njia mwafaka ya kutafuta suluhu ni kwa viongozi wa Serikali kukubali kukaa meza moja na Chadema.

Alionya kuwa endapo itaendelea na mchakato huo wa Katiba bila mwafaka, mchakato huo utakuwa umekosa uhalali wa kisiasa kitu ambacho alisema ni hatari kwa nchi. Mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini na Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni alionya kuwa bila kufikiwa kwa hatua hiyo, jambo hilo litazua mtafaruku  kwa sababu Chadema nacho kitaandaa mchakato wake wa kuunda Katiba Mpya.

 “Si lazima yote wanayoyataka Chadema yakubaliwe na wala siyo lazima yote wanayokataa upande wa Serikali ya CCM yakubaliwe. Ni lazima pande zote zikubaliane. Ni lazima ifahamike kwamba mchakato wa Katiba Mpya ni muhimu sana hivyo maridhiano ya namna ya kuipata ni jambo ambalo halipaswi kupuuzwa.”Zitto alisema tukio la wabunge wa Chadema na NCCR Mageuzi kususia muswada huo bungeni, linaonyesha kuwa wabunge wa vyama hivyo vya upinzani hawako tena tayari kushiriki kwenye mchakato huo ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakiupigania hasa baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu uliopita.
Alisema suala la kuunda Katiba Mpya ni la wananchi na wala siyo la kisiasa kama linavyopotoshwa na baadhi ya wanasiasa nchini.Kuhusu malalamiko ambayo yamekuwa yakitolewa na baadhi ya wanasiasa hasa wa CCM kuwa Chadema kina ajenda ya siri ambayo inaweza kuipeleka nchi kwenye matatizo, Zitto alisema kinachoonekana kwenye mvutano huo ni kwamba makundi mbalimbali hayaaminiani kwenye mchakato huo.Alisema katika mchakato huo:
“CCM wao wanataka kujenga mazingira ambayo yatawapa nafasi ya kuendelea kuwapo madarakani na wakati huo upinzani nao unataka yawapo mabadiliko yatakayojenga uwiano ulio sawa na unaoweza kuwapa nafasi ya kuingia madarakani.”Katika mazingira ya namna hiyo, Zitto alisema linaweza likaundwa baraza la kitaifa ambalo litashirikisha wajumbe kutoka makundi mbalimbali, hasa Serikali na viongozi wa vyama.

Alisema kamwe suala hilo haliwezi kupata mwafaka kwa kuangalia wingi wa wabunge bungeni kwa sababu hali hiyo itachukua mkono wa itikadi za kisiasa.Zitto alisema kwa mazingira ya sasa ambayo CCM ndicho chama tawala na chenye idadi kubwa ya wabunge ni rahisi suala la Katiba kutekwa kwa maslahi ya chama hicho na kusahau kuwa ni jambo linalomgusa kila Mtanzania.
Alisema mabadiliko ya Katiba ni muhimu hasa katika kipindi hiki ambacho viongozi wengi wa Serikali wamekuwa hawatekelezi wajibu wao ipasavyo na inakuwa vigumu kuwaondoa kwenye nafasi zao.Zitto alitoa mfano kuwa katika hatua za mwanzo za Kenya kutumia katiba yao mpya, imezuia uteuzi holela wa viongozi kushika nyadhifa nzito kama vile jaji mkuu na kuwaondoa baadhi ya viongozi  ambao wanatuhumiwa kwa rushwa na matumizi mabaya ya madaraka.
Kuhusu maandamano ya Chadema kwamba ni  agenda za siri zinazotaka nchi iingie kwenye migogoro na isitawalike, alisema suala la maandamano yamekuwa wakiyafanya pale kunapokuwa na ajenda maalumu ambayo inatokana na kunyimwa haki katika jambo linalowagusa wananchi wengi.Zitto alisema maandamano hayo hayafanywi ovyo kwa misingi binafsi, ila kinachotakiwa ni viongozi kutenda haki kwa mujibu wa sheria za nchi.
Mjadala bungeni
Wakati wabunge wawili wa NCCR Mageuzi wakiendelea kususia mjadala huo, Mbunge wa Kasulu Mjini kupitia chama hicho, Moses Machali alishiriki na kusema kwamba watakaoupitisha laana ya Watanzania itakuwa juu yao.Machali aliweka hadharani msimamo wake wa kutounga mkono muswada huo huku akitaja sababu za kutotoka nje ya kikao hicho kuwa ni kuwaeleza ukweli.

“Mimi sina tatizo na wenzangu wa Chadema waliotoka nje, nimebaki ndani ya kikao hiki ili kuwaeleza ukweli kuwa muswada huu ulipaswa kusomwa kwa mara ya kwanza ili tuweze kutoa fursa kwa wananchi kutoa maoni yao,” alisema Machali.Alisema kama muswada huo ungesomwa kwa mara ya kwanza ungetoa fursa kwa wananchi wengi kutoa mchango wao wa maoni ambayo yangechangia kutungwa kwa Katiba Mpya inayokidhi matakwa ya Watanzania.“Haiwezekani kukusanya maoni katika vituo vya Dar es Salaam, Dodoma na Zanzibar tukasema hayo ndiyo mawazo ya Watanzania wote. Nchi hii ni kubwa na hata ninyi wenyewe husema nchi kubwa kwani tuna haraka gani?” alisema Machali.
Mbunge wa Gando (CUF), Khalifa Suleiman Khalifa alisema: “Namshukuru Rais, juhudi hii aliyoifanya, naamini ana nia nzuri nawaomba wabunge wenzangu na Watanzania wenzangu tumsaidie kwa hili kwa sababu mwisho wa siku historia ya Katiba Mpya itaandikwa wabunge walio ndani ya Bunge hili pamoja na Rais wa Tanzania wa Awamu ya Nne.”Mbunge wa Vunjo (TLP), Augustine Mrema alisema asingeweza kutoka nje ya Bunge kwani hapo ni mahali sahihi pa kuzungumza kwa niaba ya wananchi wa Vunjo.   “Nimejaribu kuangalia kinachotufanya tugombane ni nini, tufarakane ni nini, tuelewane vibaya ni nini?

Nimeangalia hii Tume inayotaka kuundwa, Tume ya Rais, siyo mara ya kwanza nchi hii kuundwa Tume ya Rais na watu hawakufanya maandamano,” alisema akitaja Tume Jaji Francis Nyalali ya 1991 ya kuratibu maoni kuhusu mabadiliko ya Katiba na mfumo wa vyama vingi au chama kimoja na ya mwaka 1998 ya Jaji Robert Kisanga kutafuta maoni kuhusu muundo wa Muungano. Alisema kwa jinsi mchakato unavyopendekezwa, hana shaka na Katiba itakayopatikana kwani watu zaidi ya 500 watakaounda Bunge Maalumu la Katiba hawawezi kwenda kinyume cha matakwa ya umma.  

Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed alisema wabunge wa Chadema wameonyesha moyo wa ubinafsi kwa kuwadharau wabunge kutoka Tanzania Visiwani. Mbunge huyo ambaye alipata kuwa Kiongozi wa Upinzani Bungeni alikuwa akikosoa hotuba ya Msemaji wa Upinzani kuhusu Katiba na Sheria, Tundu Lissu ambayo ilionyesha wasiwasi kwamba wingi wa wabunge wa CUF katika Bunge Maalumu la Katiba linakipa chama hicho nafasi ya kuwa chama kikubwa cha pili katika Bunge hilo.

Mbunge wa Tabora Mjini (CCM), Ismail Aden Rage alilishambulia Jukwaa la Katiba Tanzania akisema limejivika uwakilishi wa wananchi na kusahau kwamba wabunge ndiyo wenye nafasi hiyo.   “Hawa watu wanasema eti wao ni wawakilishi wa wananchi, tangu lini? Wamesahau kwamba sisi ndiyo wawakilishi wa wananchi, hawa wanataka kutupokonya mamlaka tuliyopewa na wananchi,” alisema Rage.

Spika awashangaa  
Kitendo cha wabunge wa Chadema na NCCR Mageuzi kususia mjadala wa muswada huo, kimemshangaza Spika wa Bunge, Anne Makinda akisema kimewanyima haki wapigakura waliowachagua kwa lengo la kuwawakilisha.

“Siyo sawa, muswada ndiyo kwanza unajadiliwa na hapo ndipo Bunge linapotunga sheria, mimi nilikuwa natarajia kwamba kutokana na hoja zao hizo, wakati tutakapokaa kama Kamati ya Bunge zima basi kungekuwa na majedwali ya marekebisho ya sheria hii mengi, ili turekebishe lakini sasa sijui sasa hawa (Chadema) wanafanyaje mambo yao,” alihoji Makinda.

   Makinda alipuuza tuhuma zilizotolewa dhidi yake kwamba aliingilia utendaji wa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheri na Utawala na kuhoji kwamba kama tuhuma hizo ni za kweli kwa nini Lissu aliyesoma maoni ya kambi yake hakuziweka tuhuma hizo katika hotuba yake kimaandishi?

Waziri achangia Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Ummy Mwalimu alielezea kushangazwa kwake na wanaopinga muswada huo kwa kile alichodai wanaipotosha jamii.Mwalimu alitoa kauli hiyo bungeni alipopata fursa ya kuchangia mjadala  huo wa kupitisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.“Ninasikitika sana kuona wanasheria wenzangu na watu wanaojiita wanaharakati wanaohoji madaraka ya Rais.
Hawa wanaharakati na sisi wanasheria tunawajibu wa kuilinda Katiba, mnahoji Rais kuunda tume mnataka aunde nani?”“Rais ni mkuu wa nchi, siyo Mwenyekiti wa CCM tu, siyo mtu wa kawaida ndiyo maana tunasema tupitishe huu muswada na tujadili ndipo tuone.”Mwalimu ambaye ni Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), alisema Rais akiteua tume kuna makundi atakayoyaangalia yakiwamo masuala ya jinsia ambayo yako chini ya wizara yake na kuhamasisha wanawake kujitokeza kuunga mkono juhudi hizo.
NCCR Mageuzi
Katibu Mkuu wa NCCR Mageuzi, Samwel Ruhuza alisema kitendo cha Serikali na wabunge wa CCM kulazimisha muswada huo kusomwa kwa mara ya pili, ni kuwapuuza wananchi na kusema kwamba kama wataupitisha chama hicho kitawashitaki kwa wananchi.“Ule muswada uliletwa kwa mara ya kwanza ukakatiliwa, sababu za kuukataa ni kutaka ufanyiwe marekebisho na uandikiwe kwa Lugha ya Kiswahili kisha urudishwe kwa wananchi ili watu wengi waweze kuuelewa na kutoa mchango wao wa maoni.

Kama wataupitisha watakuwa wamewanyima haki Watanzania na sisi tutakwenda kuwaambia wananchi kuwa wamewapuuza.”Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba, Deus Kibamba alisema jana kwamba kupitishwa kwa muswada huo ni kuwasaliti  wananchi.“Hili ni tukio la kusikitisha hapa kwetu Tanzania. Inaonyesha sauti ya wengi siyo sauti ya Mungu, bali wachache.”
                                                                 source is www.mwananchi.co.tz                                                                                                                                                                                                         
                                 

11/15/2011

Wabunge wa Chadema na NCCR watoka bungeni.


WABUNGE wa Chadema na NCCR-Mageuzi jana walilitikisa Bunge baada ya kuungana kutoka nje ya ukumbi kupinga kile walichodai kuwa ni Spika wa Bunge, Anne Makinda kuwadharau kwa kuwanyima haki zao kwa mujibu wa kanuni.Wakati wabunge hao wakitoka bungeni kugomea muswada huo, Chama cha Majaji Wastaafu Tanzania (Tarja), kimetoa tamko kupinga hadidu za rejea za tume itakayoratibu mchakato wa kuundwa kwa Katiba Mpya kutolewa na Rais.

Licha ya Spika Makinda kuukingia kifua muswada huo katika utangulizi wake kabla ya kuruhusu uwasilishaji wa hoja kwa pande zote akisema ulifuata kanuni za Bunge, haikusaidia kwani muda mfupi baada ya Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria, Tundu Lissu kutoa maoni ya Kambi ya Upinzani, wabunge hao waliamua kuondoka.
Muswada huo wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2011, ambao uliwasilishwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani umepata pia upinzani kutoka kwa wanaharakati nchini ambao wametishia kufanya maandamano nchi nzima endapo wabunge watauridhia.
  
Tamko la Mbowe
Baadaye wabunge hao wa Chadema na NCCR Mageuzi katika tamko lililotolewa na Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe walisema: “Hatutashiriki katika mchakato wote wa mjadala wa muswada huu hadi mwisho na kesho (leo) tutaeleza hatua nyingine tutakazochukua.”
Mbowe katika mkutano na waandishi wa habari uliohudhuriwa na Wabunge wa NCCR Mageuzi, David Kafulila (Kigoma Kusini) na Felix Mkosamali (Muhambwe) alisema wamelazimika kutoka nje kutokana na Spika Makinda kuonyesha upendeleo wa wazi kwa Serikali kabla ya hata muswada huo kuwasilishwa.

“Spika ameonyesha upendeleo wa wazi kabisa kwa Serikali hata kabla ya muswada huo kusomwa na waziri, katika hali hiyo haki haiwezi kutendekeza. Hatuwezi kuunga mkono kitu ambacho kinapingwa na wananchi kote nchini,” alisema Mbowe na kuongeza:
“Shughuli nyingine za mkutano huu wa Bunge zilizobaki tutashiriki lakini hili la kujadili muswada huu hatuko tayari na lazima tupange utaratibu wa kuwafikishia wananchi.” 

Alisema upendeleo wa Spika pia ulijitokeza wakati wabunge zaidi ya watatu wa upinzani walipoomba mwongozo na yeye kukataa wakati kanuni zinawaruhusu kufanya hivyo.

“Spika anasema eti sisi tunawapotezea muda. Kuomba mwongozo si kupoteza muda, kanuni zinaturuhusu, kwa hili ametutusi lazima atuheshimu na afahamu kwamba hata sisi tumechaguliwa na wananchi,” alisema Mbowe.
Wabunge waliokataliwa na Spika walipoomba mwongozo ni Mkosamali, John Shibuda wa Maswa Magharibi (Chadema) na John Mnyika (Chadema).
Hata hivyo, wabunge wengine wawili wa NCCR Mageuzi, Mosses Machali (Kasulu Mjini) na Agripina Buyogela (Kasulu Vijijini) hawakuhudhuria kikao hicho na badala yake walibaki ndani ya ukumbi wa Bunge. Ilikuwaje?

Hali ilianza kubadilika wakati Waziri Kombani alipomaliza kuwasilisha muswada huo, kwani Mnyika alisimama na kusema: “Hoja kuahirisha mjadala,” lakini Spika alimpuuza na kumwita Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, Pindi Chana kutoa maoni ya kamati yake.
Wakati huo, Mkosamali alisimama kuomba mwongozo wa Spika lakini pia alikataliwa na Spika akisema huo haukuwa wakati mwafaka wa kuomba mwongozo kwani muda ulikuwa hauruhusu.

Chana alipomaliza kusoma maoni ya kamati, Shibuda naye alisimama kuomba kuhusu utaratibu lakini Spika hakumpa fursa hiyo, hivyo kumwita Lissu ili atoe maoni ya Kambi ya Upinzani.
Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani (kulia) na Waziri Kivuli wa Wizara hiyo, Tundu Lissu wakionyesha mabegi yao yaliyobeba hotuba ya muswada wa sheria ya mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2011, wakati wakielekea katika ukumbi wa Bunge, mjini Dodoma jana. Picha na Edwin Mjwahuzi
Baadaye Mnyika alisimama tena baada ya Lissu kuwasilisha maoni ya upinzani, lakini Spika alikataa kumpa nafasi, ndipo wabunge wa Chadema walipoinuka kutoka kwenye viti na kutoka nje.

Wakati wabunge hao wakitoka, Mkosamali alisimama akisema: “Kuhusu utaratibu,” lakini Spika alisema hakukuwa na nafasi ya kufanya hivyo na badala yake alimpa nafasi Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela (CCM) kuanza kuchangia muswada huo.

Maoni ya Upinzani
Mapema akisoma maoni ya Kambi ya Upinzani kuhusu muswada huo, Lissu alimtuhumu Spika kwamba alikuwa akiingilia Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala kinyume cha Kanuni za Bunge. 

“Spika umekuwa ukiingilia sana kamati kinyume cha kanuni za Bunge na zaidi ya hapo ulikataa ziara za kamati kwenda mikoani kukusanya maoni ya wananchi kuhusu muswada huu, hali hii haikubaliki,”alisema Lissu kauli ambayo aliirudia katika mkutano na waandishi wa habari.
Lissu alisema Spika pia alikiuka Kanuni za Bunge kwa kuongeza wajumbe watano kwenye Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala na kwamba kwa kufanya hivyo anaufanya mchakato wa sasa kuwa batili.

Alisema muswada huo ni batili kwani Serikali haikutekeleza agizo hata moja lililotolewa na Bunge kwani hata tafsiri ya muswada huo kwa Kiswahili iliwasilishwa mbele ya kamati wiki mbili zilizopita na kwamba wananchi hawakupata nafasi ya kuijadili.

“Muswada huu ni mpya, tofauti sana na ule ulioletwa hapa Aprili, hivyo kutokana na mabadiliko makubwa na kimsingi yaliyofanywa, ni dhahiri kwamba usomwe kwa mara ya kwanza ili wananchi wapate fursa ya kuujadili tena,” alisema Lissu.
Alisema mchakato wa katiba mpya unafanya makosa yaleyale ya kuendeleza mamlaka makubwa ya urais na kwamba hali hiyo inaiweka Katiba Mpya katika mikono ya Rais jambo ambali siyo sahihi.

“Kutokana na kasoro hii, ni dhahiri kwamba tutapata katiba ambayo inakidhi matakwa ya Rais, chama chake cha CCM na siyo katiba ya Watanzania, hatari ya uraisi wa kifalme kuendelea inaonekana pia hapa,” alisema Lissu.Maoni hayo pia kwa kiasi kikubwa yalichambua kasoro za ushirikishwaji wa Tanzania Visiwani katika mchakato huo na kwamba ili kuwa na msingi bora lazima kuwe na meza ya majadiliano ya kurejeshwa kwa Serikali ya Tanganyika.

Kafulila na Mkosamali
Wakizungumza kwenye mkutano wa wabunge wa Chadema, Kafulila alisema tangu mwazo hakukuwa na dhamira njema ya Spika kwani alionyesha upendeleo wa wazi kwa kuisemea Serikali.

“Kwa jambo la kitaifa kama hili, si sahihi kwa Spika kuonyesha upendeleo wa wazi, sasa kwa msimamo wangu sikuona kwa nini niendelee kukaa ndani hali kukiwa na ushahidi wa wazi kwamba demokrasia inakandamizwa,” alisema Kafulila na kuongeza:

 “Nikiwa kwenye kamati, mambo mengi yalikuwa yakifanywa ndivyo sivyo, suala la madaraka makubwa ya Rais wenzetu hawako tayari kabisa kulifanyia kazi, sasa hali hii si ya kuvumilika hata kidogo, lazima tutetee maslahi ya nchi.”

Makinda na Kombani
Mapema akiwasilisha muswada huo, Waziri Kombani alichukua muda mrefu kueleza sababu za Serikali kuamua kusoma muswada huo mara ya pili, akiwajibu wanaharakati, wanazuoni na wanasheria waliokuwa wakitoa mwito kwamba usomwe kwa mara ya kwanza kutokana na kufanyiwa marekebisho mengi.

Mapema kabla ya Kombani kusoma maelezo ya muswada huo, Spika Makinda alitoa maelezo kuhusu kuzingatiwa kwa matakwa ya kanuni ambazo zinalazimisha muswada huo kusomwa kwa mara ya pili.

Wakati akiahirisha Bunge jana, Makinda alisema kilichotokea kwa wabunge waliotoka nje ni kutotaka kutii kanuni za Bunge ambazo uongozi wake unawajibika kuzisimamia.

Kuhusu madai ya kuingilia utendaji wa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, alikiri kwamba aliwazuia wajumbe wa kamati hiyo siyo tu kwenda mikoani kukusanya maoni ya wananchi, lakini hata wale waliotaka kwenda nje ya nchi kwa lengo la kujifunza. 
“Katiba ni ya kwetu wenyewe, mnakweda nje kufanya nini?”alihoji Spika.

Msimamo wa Majaji
Tarja kimekosoa baadhi ya vifungu katika muswada huo kikiwamo kile kinachosema hadidu za rejea za Tume ya Katiba zitatolewa na Rais. Kinataka zisiwe siri ya Rais kama ilivyoanishwa katika muswada huo, bali ziwekwe wazi.

Kauli hiyo ilitolewa jana Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Tume ya Kuchambua Muswada iliyoundwa na Tarja, Jaji Mstaafu Hamisi Msumi.
“Hadidu za rejea za tume ndiyo roho ya Katiba kwa sababu ndizo zitakazoiongoza tume kutekeleza majukumu yake,” alisema Jaji Msumi alipozungumza na waandishi wa habari.

Kama kawaida Lema apokelewa kwa kishindo Arusha, baada ya kutoka jela.


SHUGHULI mbalimbali za kibiashara na kijamii katika Jiji la Arusha jana zilisimama kwa muda kupisha mapokezi ya Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema baada ya kutoka rumande katika Gereza la Kisongo alilokaa kwa siku 14.Oktoba 31, mwaka huu, Lema na wenzake 18 walifikishwa mahakamani wakidaiwa kufanya kusanyiko lisilo halali na kukaidi amri ya polisi iliyowataka watawanyike yeye na wenzake.
Walikamatwa na kufikishwa mahakamani na kudhaminiwa lakini Lema akikataa dhamana akisema ameamua kutangulia gerezani kudhihirisha kwamba haogopi gereza.Lema alitoka kwa dhamana na kuandaliwa mapokezi makubwa ya wafuasi wa Chadema ambayo yaligeuka kuwa maandamano ya amani.Shamrashamra za mapokezi hayo zilisababisha kusimama kwa muda kwa shughuli kadhaa kama huduma za kibenki hasa zile zilizo katika Barabara ya Sokoine.

Wakati wa maandamano hayo wafuasi hao wa Chadema walikuwa wakipeperusha majani na matawi ya miti.
Mahakimu, mawakili na makarani wa mahakama nao walilazimika kuacha shughuli zao kwa muda na kutoka nje kushuhudia mapokezi ya mbunge huyo yaliyokuwa yakipambwa kwa nyimbo mbalimbali nje ya mahakama hiyo.

Sehemu ya nyimbo hizo zilimgusa Mkuu wa Polisi Wilaya hiyo ya Arusha, Zuberi Mwombeji ambaye hivi karibuni aliingia kwenye mvutano mkubwa na chama hicho cha upinzani akituhumiwa kutumia nguvu kuwadhibiti viongozi wake.Waliimba: “Tunamtaka….panya wetu… tunamtaka mbunge wetu… Zuberi (OCD), aondoke. Mlituvizia usiku, leo sasa ni mchana hapatatosha. Hatuandamani, tunampokea shujaa wetu.”

Shamrashamra hizo pia ziliambatana na mabango mbalimbali huku pia kukiwa na fulana maalumu zilizokuwa zimevaliwa na baadhi ya mashabiki zikiwa na maneno yaliyosomeka: “Lema kaonyesha njia mbadala ya kudai haki. Jela ni mahali pa kuishi kama sababu ya kwenda huko ni vita
dhidi uonevu, ukandamizaji wa haki na utu wa binadamu.”

Mahakamani
Lema aliyefika mahakamani Saa 3:20 asubuhi akiwa ndani ya gari maalumu ya polisi, alipewa dhamana na Hakimu Mkazi, Judith Kamara baada ya kukamilisha masharti ya kuwa na wadhamini wawili wenye vitambulisho na barua za utambulisho ambao walisaini hati ya dhamana ya Sh5 milioni kila mmoja.

Alidhaminiwa na Sarah Mohamed na Mwajuma Manonge na kutoka eneo la Mahakama Saa 5:15 asubuhi akiwa amebebwa juujuu na wafuasi wake baada ya juhudi zake za kutaka kuondoka kwa kutumia gari lake kushindikana.Wafuasi hao walimzuia kuingia katika gari lake na kumtaka atembee kwa miguu hadi eneo la Ngarenaro ziliko Ofisi za Chadema Mkoa wa Arusha.
Mbunge huyo hakuwa na budi kukubaliana na agizo hilo la wafuasi wake kuongozana hadi Ngarenaro lakini aliwasihi wamruhusu apande na kusimama juu ya gari lake, ombi lililokubaliwa.

Licha ya mashabiki hao wa Chadema kulazimisha kumbeba Lema juujuu na kuanza kutoka naye eneo la Mahakama huku wakiimba, Kamanda wa Operesheni Maalumu za Polisi Mkoa wa Arusha, Peter Mvulla aliwaamuru askari wake waliokuwa wakilinda amani eneo hilo kutowaingilia.

“Waacheni waandamane na mbunge wao, msiwapige mabomu. Subirini tuangalie kitu gani kitatokea. Kama hawafanyi vurugu msiwaingilie hadi nitakapotoa amri nyingine. Muhimu hakikisheni mmejipanga sawasawa kila eneo,” alisikika Mvulla akitoa maelekezo kwa simu.
Busara za Mvulla aliyekuwa mkuu wa kikosi cha ulinzi katika shughuli ya jana, zilisaidia kuepusha vurugu katika mapokezi hayo yaliyoishia kwa Lema kuwahutubia wafuasi wake nje ya ofisi za chama hicho mkoa huku amani na utulivu vikitawala.

Mkutano hadhara
Akihutubia umati mkubwa wa watu nje ya ofisi hizo, Lema alisema Serikali isidhani kuwa ina uwezo kutumia dola kusaidia CCM Arusha na kuonya kwamba, yuko tayari kujiuzulu nafasi yake ili kuruhusu uchaguzi mdogo akiahidi kunyakua tena kiti hicho kwa kura zaidi ya 56,196 alizopata kwenye uchaguzi uliopita.

“Maisha yangu siyo kwa ajili ya kuishi leo, bali kufa kwa faida. Ndiyo maana kila siku nasema ni heri vita inayotafuta haki, kuliko amani inayopumbaza na kudhalilisha utu wa mtu,” alisema huku akishangiliwa.Alisema jana usiku alipanga kuelekea Dodoma kuhudhuria kikao cha Bunge kushiriki mjadala wa Katiba Mpya akionya kuwa iwapo kutakuwapo uchakachuaji ataanzisha balaa jingine kubwa kuliko la Arusha.

Amjia juu RC
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya maandamano hayo, Lema alisema suluhu ya mgogoro wa Arusha utapatikana kwa uchaguzi wa umeya kurudiwa na kumuonya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo kuacha kudandia gari asilojua linakoelekea akimaanisha mgogoro unaoendelea.
“Bila haki kupatikana, sasa tutaanza maandamano kwenda majumbani mwa viongozi wanaokandamiza haki zetu. Waandae risasi na mabomu ya kutosha kwani mapambano ndiyo kwanza yameanza. Eti RC anauliza kwa nini hatuandamani sehemu nyingine, tukaandamane sehemu kama Tabora ambako hakuna sababu ya kufanya hivyo? Arusha tuna sababu ya kuandamana,” alisema Lema.

Kuhusu kauli aliyodai ya vitisho kutoka kwa Mulongo aliyeonya wanaopanga kuvuruga amani na utulivu Arusha, Lema alisema kiongozi huyo bado anakabiliwa na ugeni ndiyo sababu anatoa kauli bila kuzifanyia utafiti.

Jiji la Arusha limekuwa likigubikwa na vurugu za kisiasa mara kwa mara tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana ambao pamoja na mambo mengine, uliacha majeraha yanayotokana na matokeo ya uchaguzi wa umeya ambao Chadema umekuwa ukiyapinga.